Ripoti: Vitendo vya ukatili vyaongezeka nchini, Dar es salaam yaongoza

Watu 479 wameuawa nchini kutokana na vitendo vya ukatili ukiwamo wa watu kujichukulia sheria mkononi katika kipindi cha nusu mwaka 2017, ikiwa ni mara tatu ikilinganishwa na mwaka uliopita, jambo linaloonesha kuwapo ukiukwaji wa haki.
Akisoma ripoti ya hali ya haki za binadamu nchini Tanzania jana mbele ya Waandishi wa Habari, 
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dkt Helen Kijo Bisimba amesema Mkoa wa Dar es Salaam unaongoza kwa watu kujichukulia sheria mkononi kwa kuwa na matukio 117 yaliripotiwa polisi, ukifuatiwa na Mkoa wa Mbeya wenye matukio 33, Mara (28) na Geita (26).
Ripoti hiyo inaonesha hali ya haki za binadamu kuwa bado ni mbaya kwa kipindi cha nusu mwaka ikilinganishwa na miaka iliyopita.
Dk Bisimba alisema ripoti hiyo inayoanzia Januari hadi Juni mwaka huu inaonesha kuwepo kwa ukiukwaji mkubwa wa haki za kiraia hususani haki ya kuishi, lakini pia ukiukwaji mkubwa wa haki za makundi maalumu wakiwemo wanawake na watoto.
Kuhusu kujichukulia sheria mkononi, Dkt Bisimba amesema taarifa za Jeshi la Polisi zinaonesha kuwa matukio ya mauaji kwa watu kujichukulia sheria mkononi yamekuwa yakipungua kuanzia mwaka 2013 mpaka 2016 kutoka vifo 597 mpaka vifo 135.
“Hata hivyo, matukio hayo imeonekana kujirudia tena kwa kasi ambapo na kufikia mara tatu ya idadi ya mwaka jana,” amesema Dkt Bisimba.
Hata hivyo, Dkt Bisimba amesema Jeshi la Polisi linapaswa kushughulikia haraka tatizo la kuwapo matukio hayo na kuhakikisha watuhumiwa wanafikishwa mbele ya sheria huku akiishauri Wizara ya Mambo ya Ndani na Jeshi la Polisi kwa pamoja kuhakikisha kuwa askari wanaotuhumiwa kufanya mauaji ya raia wanachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.
Kuhusu haki za wanawake na watoto Dkt Bisimba amesema matukio ya ukiukwaji wa haki za makundi hayo yameendelea kuripotiwa kwa kiwango kikubwa nchini na taarifa ya Jeshi la Polisi kwa kipindi cha Januari hadi Machi, inaonesha kumekuwa na matukio 2,059 ya ubakaji yaliyoripotiwa katika vituo mbalimbali.
Mtafiti wa LHRC, Fundikila Wazambi amesema ripoti hiyo inatokana na tafiti mbalimbali zilizofanywa na kituo hicho wenye lengo la kuangalia ukiukwaji wa haki za binadamu.

No comments

Powered by Blogger.