Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Arusha (CCM), Catherine Magige ''Cathy'' na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Alex Ntibenda waibua Mapya!

DAR ES SALAAM: Siku chache baada ya Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Arusha (CCM), Catherine Magige ''Cathy'' kutoa ya moyoni kuhusu madai yaliyosambaa ya kutoka kimapenzi na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Alex Ntibenda, bosi huyo ameibuka na kutoa tuhuma kali zinazosababisha sasa viongozi hao wawili kuwa katika vita nzito, Risasi Mchanganyiko linaweza kuripoti. Awali, gazeti pacha na hili, Risasi Jumamosi lilipenyezewa habari kwamba wawili hao hawako sawa, baada ya kudaiwa kutofautiana kwa sababu za kimapenzi, huku wengine wakidai kuwa tuhuma za kuharibiana kazi baina yao, ndiyo hasa chanzo cha mzozo. Aidha, baadhi ya vyanzo vya kuaminika jijini Arusha vinadai kuwa uchaguzi mkuu wa ndani wa Chama Cha Mapinduzi ndicho chanzo kikubwa cha mzozo huo.
SAKATA LILIVYOANZA
Awali kabla ya Ntibenda kuachishwa kazi na Rais Dk. John Magufuli, Cathy aliilalamikia Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, ambayo huwa chini ya mkuu wa mkoa, kwamba imeshindwa kudhibiti suala la shule kuchomwa moto mkoani humo kila kukicha. Lakini baadhi ya watu wakasema, Cathy anamtuhumu Ntibenda kwa sababu walikuwa na uhusiano wa karibu sasa umetibuka. Lakini kuhusu madai hayo, Cathy alisema: Haiwezekani shule zikawa kila siku zinaungua, hapa kuna tatizo, Kamati ya Mkoa ya Ulinzi na Usalama inapaswa kuwajibika, maana inaonekana haifanyi kazi yake kwa ufasaha. Alipoulizwa kuhusu madai ya kuhusika kwake katika kuondolewa kazini kwa Ntibenda, Cathy alisema yeye alizungumza kuhusu kamati hiyo kushindwa kuwajibika, hivyo haifai na kwamba kama kwa kusema hivyo kumesababisha aondolewe, ni sawa maana alitimiza wajibu wake kama kiongozi. Haiwezekani bwana kila siku shule zinachomwa, ukiuliza kamati ya ulinzi na usalama inafanya nini? Hakuna majibu ya kueleweka. Tunataka kupeleka misaada lakini tunashindwa maana hata ukipeleka, shule zinachomwa katika staili ileile.Mimi nilisema kama mzazi na nilisema hadharani kama kiongozi. Kama ametimuliwa kwa sababu ya yale niliyosema pia ni sawa tu, alifunguka Cathy. 
HAPO NDIPO NTIBENDA UZALENDO ULIPOMSHINDA
 Lakini Ntibenda ambaye wiki iliyopita kwenye Risasi Jumamosi hakuweza kupatikana na hivyo gazeti kuficha utambulisho wake, safari hii alipatikana kupitia simu yake ya mkononi, lakini awali alikuwa mgumu kuzungumzia suala hilo, akidai hataki tena kujihusisha na siasa za Arusha zaidi ya kuwa mjasiriamali. Kama unataka kuzungumza na mimi kuhusu masuala ya ujasiriamali karibu, lakini kama ni mambo ya siasa za Arusha mimi siko tayari kuzungumzia, alisema Ntibenda ambaye wakati huo alisema yupo jijini Dar kwa shughuli zake za kijasiriamali. Wakati kiongozi huyo akikata simu alisisitiza msimamo wake, mwandishi wetu aliamua kumtumia ujumbe mfupi wa maandishi, uliosomeka: Kuna taarifa tumepata kwamba kuondolewa kwako kule kwenye ukuu wa mkoa kumesababishwa na mbunge Cathy Magige, ni kweli? Muda mfupi baadaye, Ntibenda alirudi hewani na kuamua kutoa dukuduku lake, akimtupia tuhuma mbunge huyo kuwa yeye, pamoja na Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Mkoa wa Arusha, Lengai Ole Sabaya, walikuwa wakiendesha kampeni za kumhujumu ili aonekane hawezi kufanya kazi. Yeye (Cathy) anawajua waliokuwa wakichoma mashule, juhudi zangu kama mkuu wa mkoa zinajulikana, watu wanazijua, watu walifanya vile ili nionekane sifai. Kwani yeye mkimuuliza anasemaje? Muulizeni yeye (Catty) alifanya nini na kwa nini hadi mimi nikafukuzwa. Maana yeye alikuwa akisema anakula na wakubwa na kwamba ananipa siku na kweli nikaondolewa kazini. Maana mimi najua yeye anajua kila kitu, alikuwa akishirikana na Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana (UVCCM) wa , Sabaya), walikuwa wanaelewana, muulizeni yeye atawapa majibu.

VIPI KUHUSU MISAADA MASHULENI? 
Kuhusu madai ya Cathy kuwa kuchomwa kwa shule hizo kulimzuia yeye kutoa misaada, Ntibenda alisema Cathy hakuwa akitoa msaada wa aina yoyote. Cathy hakuwa akitoa msaada wowote. Mimi ndiye niliyekuwa nikitoa misaada. Muulizeni vizuri (Cathy), yeye ndiye anajua, alisema Ntibenda. 

HUYU HAPA MWENYEKITI WA UVCCM 
Lengai Ole Sabaya, Mwenyekiti wa UVCCM Arusha, alipatikana kupitia simu yake ya mkononi na baada ya kumsomea tuhuma zote dhidi yake zilizotolewa na kiongozi wake huyo wa zamani, alifunguka: Alifukuzwa kazi kwa sababu ya uzembe, uzembe wa kwanza ni kushindwa kuwatambua watu waliokuwa wakichoma moto mashule, kama anasema mimi na Cathy tunawajua, basi utakuwa ni uzembe mwingine wa pili kwa sababu alishindwa kutukamata wakati anajua sisi tunawajua. Mwambie Ntibenda, tuna ushahidi wa mambo yake mengi aliyokuwa akiyafanya ikiwa ni pamoja na kukihujumu chama, huyu alikuwa akikutana na madiwani wa upinzani na kuweka nao mikakati, ndiyo maana baada ya kutimuliwa, Chadema walikuwa wa kwanza kulalamika. 

KUHUSU MAPENZI 
Katika gazeti la Risasi Jumamosi iliyopita, Mbunge huyo wa Arusha kupitia viti maalum, alitoa ufafanuzi wa madai ya watu kwamba alikuwa akitoka kimapenzi na mkuu huyo wa mkoa, wakidai ndicho kilikuwa chanzo cha tofauti zao za sasa. Hata hivyo, Cathy alikanusha madai hayo, sambamba na Ntibenda mwenyewe aliyesema hajawahi kujihusisha na mrembo huyo, kwa vile mumewe ni rafiki yake na anamchukulia Catty kama shemeji yake. Mimi sijawahi kuwa na uhusiano na Cathy, kwanza mumewe ni rafiki yangu mimi, tuko vizuri. 

CATHY TENA
 Juzi, Risasi Jumatano lilimpigia tena simu Catty na kumpa majibu ya Ntibenda ambapo aliishia kusema: Mimi ndiyo najua mimi! Muulizeni vizuri. (akatata simu). Habari hii ilitoka kwa mara ya kwanza katika gazeti la Risasi Jumamosi, wiki iliyopita ikiwa na kichwa cha habari; MBUNGE CATHY AFUNGUKA MAZITO
chanzo 2jiachie.com

No comments

Powered by Blogger.