LIPUMBA AKWAMA KUFUTA KESI INAYOMZUIA KUPEWA RUZUKU YA CUF

Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imekataa maombi ya Mwenyekitti wa CUF anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Profesa Ibrahim Lipumba na wenzake, ya kufuta kesi namba 28/2017 inayomzuia kupata ruzuku ya chama hicho. 
Kupitia taarifa yake kwa umma aliyotoa leo Agosti 17, 2017, Naibu Mkurugenzi wa Habari, Mawasiliano na Umma CUF, Mbarala Maharagande amesema Jaji wa Mahakama Kuu, Wilfred Ndyansobera anayesimamia kesi hiyo, amekataa maombi hayo ya Lipumba ambaye ni mshitakiwa kwenye kesi hiyo.
Kwa mujibu wa Maharagande, kufuatia maamuzi hayo ya mahakama, Prof. Lipumba na wenzake watakosa kiasi cha shilingi bilioni 1.4 ambazo zilikuwa ruzuku ya chama hicho mpaka mwishoni mwa mwezi Julai mwaka huu. 
Kesi hiyo ilifunguliwa na Bodi ya Wadhamini ya CUF inayomuunga mkono Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Shariff Hamad baada ya Lipumba kupewa ruzuku ya chama hicho na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa. Ambapo Bodi hiyo inadai kuwa uamuzi huo ulikuwa kinyume cha sheria kwa madai kuwa Lipumba si kiongozi halali wa chama hicho.
chanzo ;dewjiblog

No comments

Powered by Blogger.