YANGA YAMPIGA CHINI BEKI, SABABU HIZI HAPA

                         Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa Yanga, Dismas Ten.

YANGA imeachana na beki raia wa Nigeria, Yisa Anifowoshe ambaye alikuwa akifanya majaribio kikosini hapo akitokea Al Ittihad ya Oman.
Beki huyo alikuwa akipewa nafasi ya kuziba pengo la Mtogo, Vincent Bossou, lakini akashindwa kulishawishi benchi la ufundi hivyo akakosa ulaji.

Akizungumza na Championi Jumamosi, Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa Yanga, Dismas Ten, alisema benchi la ufundi la timu hiyo chini ya kocha mkuu, George Lwandamina raia wa Zambia, liliamua kuachana na beki huyo baada ya kubaini ana uwezo mdogo.

“Yule Mnigeria hakusajiliwa kwa sababu hakuwaridhisha watu wa benchi la ufundi, aliachwa Dar es Salaam wakati wenzake wanakwenda Pemba kuweka kambi.

“Mpaka usajili wa wachezaji wa kimataifa unafungwa Agosti 15, sisi tulikuwa na wachezaji sita tu wa kimataifa ambao ndiyo tutawatumia mpaka kipindi kijacho cha usajili kama kutakuwa na uwezekano wa kuongeza mtu mwingine,” alisema Ten.

Hadi sasa wachezaji wa kigeni Yanga ni Youthe Rostand wa Cameroon, Donald Ngoma na Thabani Kamusoko wote kutoka Zimbabwe, Obrey Chirwa (Zambia), Amissi Tambwe (Burundi) na Papy Tshishimbi kutoka DR Congo.

No comments

Powered by Blogger.