Wakala aondoa utata wa safari ya Farid Musa (Azam FC) Hispania

Wakala wa kiungo wa Azam FC, Farid Mussa anayesimamia dili lake la kwenda kucheza soka nchini Hispania, John Solzano, amemaliza utata uliopo juu ya safari yake.
Solzano ambaye ni raia wa Hispania, amesema kila kitu kimekamilika na kinachomchelewesha Farid kwenda kujiunga na Tenerife inayoshiriki ligi daraja la kwanza Hispania ni kukosa kibali cha kufanya kazi nchini humo na si kingine.
Tangu Farid afuzu majaribio ya kujiunga na timu hiyo kwa mkopo, kumekuwa na maneno mengi miongoni mwa hayo ni kwamba Azam FC inambania kijana huyo kwenda kucheza soka la kulipwa.
Akizungumza na kituo kimoja cha redio, siku ya Jumatatu, Solzano alisema “Watu wanatakiwa kufahamu kwamba Farid atajiunga na Tenerife kwa mkopo, kwa sasa kinachomkwamisha asijiunge na timu hiyo ni kukosa kibali cha kufanyia kazi nchini Hispania ambacho tunaamini kabla ya mwaka huu haujamalizika kila kitu kitakuwa sawa. Tofauti na hapo hakuna kingine kinachomzuia asijiunge na timu hiyo.”
Wakati wakala huyo akiyasema hayo, naye Meneja Mkuu wa Azam FC, Abdul Mohammed, alisema: “Tayari tumetoa ITC yake, hivi unadhani kama tungekuwa hatutaki aondoke tungeweza kuitoa?
“Niseme tu hakuna mtu aliyemzuia Farid kwenda Hispania, kila mmoja hapa klabuni kuanzia ngazi ya juu mpaka chini tunafanya juhudi za dhati kabisa kuona dili hilo linakamilika haraka iwezekanavyo.
“Mamlaka ya Uhamiaji ya Hispania ndiyo inatoa hicho kibali cha kazi, hivyo suala la Farid ndiyo limekwamia hapo, sisi Azam na Ubalozi wa Hispania hapa nchini tumemaliza kila kitu kwa yale yanayotuhusu, kilichobaki ni huko huko Hispania.”

No comments

Powered by Blogger.