ABDULRAHMAN: WAONGO SIUMWI, HAWATAKI KUNIITA TU STARS

Mchezaji wa Ruvu Shooting, Abdulrahman Mussa (kulia) akifanya yake.
MFUNGAJI bora wa msimu uliopita kwenye Ligi Kuu Bara, Abdulrahman Mussa, ameibuka na kusema anashangazwa na taarifa kuwa yeye ni majeruhi na ndiyo maana hajaitwa Taifa Stars.
Wiki iliyopita Kocha wa Stars, Salum Mayanga alitangaza kikosi ambacho kinashiriki Michuano ya Chan ambayo inahusisha wachezaji wa ligi za ndani huku jina la mkali huyo wa mabao likiwa halipo na kusababisha wadau kuhoji.
Akizungumza na Champion Jamatatu, Abdulrahman alisema anashangazwa na taarifa zinazosambazwa na (anamtaja) kuwa yeye ni majeruhi jambo ambalo siyo kweli kwani ni mzima na anaumizwa na jambo hilo kwani anatamani kuichezea timu ya taifa lakini hajapata nafasi hiyo.
“Nimefanya vyema kwenye ligi kuu, mie siyo majeruhi, imeniuma sana sasa kwa nini mtu aongee hivyo wakati siyo, ni bora angetaja sifa nyingine labda sifai katika mfumo wa kocha au mambo mengine lakini siyo kunisingizia ugonjwa.
“Mimi baada ya kusikia taarifa hizo nikampigia daktari wa timu ya taifa nikamuuliza kama kweli ninaumwa maana tulikuwa wote kwenye kambi ya Stars kule Misri akaniambia hapana nipo sawa, basi nikatulia kwa kuwa huwezi kulazimisha kucheza Stars japokuwa ninatamani nichezee taifa langu.
“Mie nataka kucheza Stars ili niisaidie timu na pia kujiuza nje. Unajua ukicheza Stars CV (wasifu) yako inaongezeka na hata ukipata timu nje hawaangalii takwimu za klabu yako, wanakuangalia kama unacheza na timu ya taifa,” alisema Abdulrahman.
Championi lilimtafuta Kocha wa Stars, Mayanga azungumzie ishu ya kutomuita Abdulrahman Mussa kikosini mwake lakini simu yake haikupokelewa.

No comments

Powered by Blogger.