WAZIRI MWIGULU AKWEPA KUVAA JEZI YA SIMBA KIUJANJA, MASHABIKI WADAI KISA NI YANGA

Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba ambaye inajulikana wazi kuwa ni shabiki mkubwa wa Yanga, jana Jumanne alijikuta akilazimika kuvaa fulana nyekundu ambayo ilimfanya aonekane kama Mwanasimba.
Tukio hilo lilitokea wakati Waziri Mwigulu alipokuwa ameambatana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Muungano na Mazingira, Januari Makamba ambaye alikuwa mgeni rasmi katika Tamasha la Simba Day.
Akiwa na kitamba chake chenye rangi ya bendera ya Tanzania shingoni, Waziri Mwigulu hakuvaa jezi ya Simba bali alivaa fulana nyekundu ambayo ina rangi kama inayotumiwa na Simba ambao ni wapinzani wa jadi wa Yanga.
Kutokana na hali hiyo baadhi ya mashabiki waliokuwepo kwenye Uwanja wa Taifa, walijikuta wakitabasamu na kusema Mwigulu amekwepa kuvaa jezi ya Simba na kuamua kuvaa fulana yenye rangi nyekundu kutokana na upinzani wa jadi baina ya timu hizo.
Licha ya kujulikana kuwa ni shabiki mkubwa wa Yanga, lakini kwa sasa Mwigulu ni mdau mkubwa wa Singida United.

No comments

Powered by Blogger.