NIYONZIMA ALIYOWAKWEPA YANGA AIRPORT

                                                  Haruna Niyonzima alivyotua nchini.

KIUNGO mpya wa Simba, Mnyarwanda, Haruna Niyonzima alitua nchini jana alfajiri akitokea kwao Rwanda tayari kwa kujiunga na kikosi cha timu hiyo kwa ajili ya maandalizi yake ya msimu ujao.
Hata hivyo, mara baada ya kutua nchini viongozi wa Simba walilazimika kutumia mbinu za kimafia kumtoa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) baada ya kubaini kuwepo kwa mashabiki wa Yanga ambayo ilikuwa ni timu yake ya zamani.
Habari za kuaminika kutoka ndani ya Simba zimedai kuwa viongozi wa klabu hiyo waliofika uwanjani hapo kumpokea, walibaini uwepo wa mashabiki hao na nia yao kubwa ilikuwa kumfanyia fujo kwa kile ambacho kinadaiwa ni kukasirishwa na kitendo cha kuhama kwenye timu yao na kwenda kwa watani wa jadi.
Kiongozi mmoja wa Simba ameliambia gazeti hili kuwa walilazimika kuwasiliana na uongozi wa uwanja huo wa ndege na kuwaeleza juu ya mkakati uliokuwa umepangwa kabla ya Niyonzima kutoka ndani ya eneo la ukaguzi.
“Ilitubidi tumpitishie VIP, tuliomba kwenye mamlaka za uwanja, wakaturuhusu, ilivyokuwa hivyo tukampitisha huko kisha akaingia kwenye gari na tukaondoka naye, tukawaacha mashabiki hao wa Yanga uwanjani hapo.
“Niyonzima alitua nchini na ndege ya saa tisa alfajiri ya leo (jana) na tukaenda kumficha sehemu kabla ya kuungana na wachezaji wenzake kwa ajili ya mazoezi ya kujiandaa na msimu ujao wa ligi kuu,” kilisema chanzo hicho cha habari.
Katika hatua nyingine, mshambuliaji wa Simba raia wa Ghana, Nicolas Gyan naye aliyetegemewa kuwasili nchini jana usiku ili kumalizia masuala ya usajili wake na Simba na kuna uwezekano mkubwa akawa mmoja wa wachezaji watakaotambulishwa katika Simba Day, kesho Jumanne.

No comments

Powered by Blogger.