SOMA TEGETE ALIVYOWATISHA WEKUNDU WA MSIMBAZI

MSHAMBULIAJI wa Mwadui FC Jerryson Tegete amekiri mchezo wa leo dhidi ya Simba utakuwa mgumu kwavile wapinzani wao wapo kwenye kiwango bora huku wao wakihitaji ushindi kwa hali yoyote baada ya kukusanya pointi nane kwenye michezo yao minne ya mwisho iliyoshuka dimbani.

Tegete alisema matokeo hayo yamewaongezea morali wachezaji katika mchezo huo utaofanyika kwenye uwanja wa Kambarage mkoani Shinyanga ambapo kwa pamoja wameamua kuisimamisha Simba ambao katika michezo yao 11waliyocheza hawajapoteza mchezo hata mmoja na kutoka sare miwili pekee.

Akizungumza na BOIPLUS Tegete alisema kuwa timu yao imeanza kurudi kwenye mstari baada ya kuyumba katika mechi kadhaa zilizopita na sasa kuelekea kumalizika kwa mzunguko wa kwanza wamejipanga kuhakikisha kumchapa kila atakayepita mbele yao wakianza na Simba.

“Lolote linaweza kutokea tulikuwa katika kipindi kigumu lakini sasa timu imeanza kukaa sawa kama umeona mechi zetu nne za mwisho tumetoka sare mbili na tumeshinda mbili, mechi ya tano ni dhidi ya Simba nayo tumejipanga kufanya vizuri,”  alisema Tegete.

Tegete ambaye alikuwa akiifunga Simba mara kwa mara wakati akiichezea Yanga alisema tangu aondoke Yanga amecheza mechi moja tu dhidi ya Wekundu hao  msimu uliopita na hakufanikiwa kuwafunga ila kama atapewa nafasi ya kucheza kesho itakuwa ngumu kwa safu ya ulinzi ya Simba kumzuia asicheke na nyavu.

Mwadui imefunga mabao 9 tu katika michezo 11 hali inayoashiria kuwa hawana safu imara ya ushambuliaji huku Simba wakiruhusu nyavu zao kutikiswa mara tatu pekee kitu kinachompa ugumu Tegete kupita kwenye safu hiyo ngumu iliyo chini ya Method Mwanjale na Juuko Murshid.

No comments

Powered by Blogger.