Rufaa ya Tigo yagonga mwamba, watakiwa kuwalipa AY na Mwana FA Bilioni 2.1

Mahakama Kuu ya Tanzania imetupilia mbali rufaa iliyofunguliwa na kampuni ya Tigo kupinga kuwalipa wasanii AY na MwanaFA shilingi 2,185,000,000 (zaidi bilioni mbili) kwa kutumia nyimbo za wasanii hao bila kuwalipa.
Wakili wa wasanii hao, Albert Msando amesema huu ni ushindi muhimu kwa sanaa ya Tanzania, kuongeza kuwa “ni haki yao kulipwa kwa sababu ni kazi zao ambazo zinalindwa kisheria”.
Ikumbukwe kabla ya rufaa ya Tigo, mwaka jana Mahakama Wilaya ya Ilala, iliamuru kampuni ya MIC Tanzania (Tigo) kuwalipa wasanii hao kiasi hicho cha fedha kutumia nyimbo zao bila idhini. Kampuni hiyo ilibainika kutumia nyimbo za wasanii hao kwa kipindi tofauti kama miito ya wateja wao na kufanya biashara bila idhini ya wasanii husika.
Hakimu Mkazi Mwanadamizi wa Mahakama ya Ilala, Juma Hassan alitoa hukumu hiyo April 11 mwaka jana, baada ya kuendeshwa kwa kesi hiyo kwa kipindi cha miaka minne. Mbali na shilingi bilioni 2, Tigo waliamriwa kuwalipa wasanii hao shilingi milioni 25 zingine.

No comments

Powered by Blogger.