Simba SC kufukuza wachezaji wake tano wa kigeni

                                     Mshambuliaji wa Simba Mrundi ‘Laudit Mavugo’ 
 Wanamsimbazi na hata baadhi ya viongozi mpaka sasa hawaamini kama timu yao ndio imeukosa ubingwa wa Ligi Kuu Vodacom Tanzania Bara msimu huu, lakini moja ya wajumbe wa Baraza la Wadhamini wa klabu hiyo, Hamis Kilomoni amefichua siri nzito kuwa kuna wachezaji watano wa kigeni watatemwa na klabu hiyo.
Kilomoni amesema kuna wachezaji watano wa kigeni watatemwa klabuni hapo ili kupisha wazawa kuipigania klabu hiyo kwani wanagharama ndogo na wanajitoa kuipigania timu kwa jasho na damu.
 Kilomoni aliyewahi kuwa mchezaji na kiongozi wa Simba kabla ya kuwa Mwenyekiti wa Baraza la wadhamini, alisema Simba haikupata huduma sahihi kwa nyota wake saba wa kigeni iliowasajili msimu huu kwa uwezo mdogo walionao, hivyo anaona ni bora idadi yao ipunguzwe ibaki wawili tu.
Alisema mabosi wa Simba walifanya kosa kubwa kuwadharau wachezaji wazawa na kuwakimbilia wageni ambao wamekuwa hawana msaada wowote zaidi ya kuitia gharama kubwa ya kuwahudumia.
                                                                   Timu ya simba
Tulikuwa na wachezaji wengi kutoka kikosi B, lakini sijui nini kilitokea wakatolewa, huko waliko wanafanya vyema na hata kuisumbua Simba, halafu sisi tukakimbilia wageni saba ambao ukiniuliza faida yake hata sijaiona, nafikiri tunapaswa kuangalia upya hili suala la wachezaji wa kigeni halisaidii soka letu, Simba kama kuna wachezaji wa kigeni wanaostahili kubaki na walioisaidia timu wako wawili tu hawa wengine sioni wanachokifanya.” Alisema Kilomoni.
Hata hivyo Kilomoni hajawataja nyota wanaostahili kusalia, japo Simba kwa sasa ina wachezaji wa kigeni ambao ni  Method Mwanjali, Juuko Murshid, Fredrick Blagnon, Janvier Bokungu, Laudit Mavugo, James Kotei na kipa Daniel Agyei.
Chanzo : Mwanaspoti

No comments

Powered by Blogger.