Afya ya Rais Mugabe Yazua Utata

Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe, yuko nchini Singapore kwa ajili uchunguzi wa afya yake, huku maofisa wa serikali wakikanusha taarifa za kiongozi huyo kuzidiwa,

Kwa mujibu wa gazeti la serikali la Sunday Mail Rais Mugabe aliondoka nchini humo Ijumaa wiki iliyopita kuelekea nchini Singapore kwa matibabu na kwamba kiongozi huyo anatarajiwa kurejea katikati ya wiki hii.

Safari za rais Mugabe nchini Singapore zimeongezeka kwenye miaka ya hivi karibuni ambapo mara ya mwisho kuwa nchini humo ilikuwa ni mwezi Mei ambapo pia alisafiri kwa sababu za kimatibabu na mwaka 2011 na 2014 alifanyiwa upasuaji wa jicho.

Afya ya Rais Mugabe imeendelea kuzua mijadala nchini mwake ambapo mwezi Machi mwaka huu mamlaka nchini humo ziliwakamata waandishi wa habari wawili walioandika kuwa afya ya kiongozi huyo imezorota.

Licha ya umri alionao, chama chake cha ZANU-PF mwaka jana kilimteua kupeperusha bendera ya chama hicho kwenye uchaguzi mkuu ujao, huku kukiripotiwa mgawanyiko ndani ya chama hicho.

No comments

Powered by Blogger.