Rafiki wa Mashali aeleza alichozungumza na Mashali wakati yupo hospitali

Rafiki wa karibu wa marehemu Thomas Mashali aliyejitambulisha kwa jina la Ally amesimulia mkasa mzima wa kifo cha rafiki yake huyo.
Ally alisimulia mkasa wa rafiki yake huyo akiwa msibani maeneo ya Tandale jijini Dar es salaam, ambapo amedai kuwa juzi usiku alipata taarifa za kushambuliwa kwa Mashali na watu wasifahamika maeneo ya Kimara jijini humo.
“Ilikuwa usiku nimekaa nyumbani Manzese Midizini akaja dereva wa bodaboda anaitwa Yusuf Kidevu akaniambia babaako wanampiga huko Kimara wanamuua kama vipi nenda.”
“Nikahisi ni uongo kwasababu wakati mwingine wanazusha tu, mara kidogo akaja mtu wa pili akasema babaako anakufa huko Kimara, kwasababu alikuwa ni mtu wa pili kuniambia nikaona bora niende.”
“Nikaenda hadi Kimara, kufika pale nikakuta wameshampiga wamemuumiza askari wanampakia kwenye gari. Nikalifata gari hadi Sinza, akapata kitanda akalazwa nikaenda kumsalimia lakini sauti ilikuwa inatoka kwa mbali hadi usogeze sikio ndio unaweza kumsikia.”
“Nikamuuliza imekuwaje, akasema kuna dereva bodaboda alimkodi lakini walivyofika Kimara akampa hela kidogo wakaanza kuzozana ndio mkasa ulipoanzia.”
“Alimpa shilingi 2000 lakini dereva bodaboda alikuwa anataka shilingi 3000, akaanza kumtukana Mashali akaona anadharauliwa akampiga ngumi yule dereva bodaboda akaanguka chini, baada ya hapo akaanza kupiga kelele za mwizi wakaja watu wengine watatu wakataka kumpiga akapambana nao akawapiga.”
“Baada ya kuona wote hawamuwezi wote wakaanza kupiga kelele za kumuita mwizi, wakaongezeka watu wengine wakaanza kumshambulia.”
Mwili wa Thomas Mashali unatarajiwa kuzikwa Jumatano jijini Dar es salaam.
Source: Shaffih Dauda

No comments

Powered by Blogger.